Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini KKKT Atoa Ujumbe wa Mwaka Mpya 2026
Moshi – Mkuu wa Dayosisi ya Kaskazini ya Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Dk Fredrick Shoo amewataka waumini na Watanzania kwa ujumla, kuuanza Mwaka Mpya wa 2026 kwa imani, shukrani na matumaini mapya, akisisitiza kuufikia mwaka huu mpya ni neema ya Mungu na siyo kwa nguvu wala uwezo wa mwanadamu.
Akitoa ujumbe wake wa Mwaka Mpya kwa wanadayosisi ya Kaskazini, Alhamisi Januari 1, 2026, Dk Shoo amesema licha ya changamoto mbalimbali zilizojitokeza mwaka 2025, waumini hawapaswi kukata tamaa bali wamtegemee Mungu aliye mwaminifu, mwenye uwezo wa kufanya mambo yote kuwa mapya.
"Wapendwa wanadayosisi, Sio kwa nguvu wala kwa uwezo wetu. Tumejaliwa kuuona Mwaka Mpya huu wa 2026. Ni kwa neema tu. Sifa, shukrani na utukufu ni kwa Mungu wetu. Ninawaombea wote, Mungu aliyetupa neema hii atujalie Mwaka wenye neema na baraka tele," amesema Dk Shoo.
Amehimiza wananchi kumtazama Mungu pekee hata katika hali ngumu, wanazopitia kimaisha akirejea maandiko yanayosema, "Tazama, nayafanya yote kuwa mapya" (Ufunuo wa Yohana. 21:5).
"Bila kujali tumepitia hali gani 2025, tuuanze mwaka huu tukiamini kuwa Mungu wetu ni mwaminifu; Tukimtegemea na kuliitia Jina lake, yeye atatutendea mambo makuu. Hata kwa yale tunayoona yamekuwa magumu, au yameshindikana, tumtazame yeye tu," amesema.
Wito wa Mabadiliko ya Kiroho na Kimaadili
Dk Shoo ameomba 2026 uwe mwaka mpya kiroho na kimaadili kwa Kanisa, viongozi na taifa kwa ujumla, akisisitiza umuhimu wa mioyo mipya iliyojaa unyenyekevu, upendo, uvumilivu, amani na haki.
Amesema Mungu ana uwezo wa kuponya mioyo iliyojeruhiwa, iliyojaa huzuni, chuki, visasi na kukata tamaa, kwa mujibu wa ahadi yake.
"Mioyo iliyojeruhika, iliyo na huzuni, iliyokata tamaa, iliyojaa kiburi, chuki, visasi na kutokujali ikafanywe upya, maana huyu Mungu aliyetupa neema ya Mwaka mpya anao uwezo huo asemapo, ‘Nami nitawapa ninyi mioyo mipya,’ (Ezekieli 36:26)," amesema Dk Shoo.
Ameongeza kuwa, "Mungu atujalie sote mioyo mipya yenye unyenyekevu, uvumilivu, ujasiri na uthubutu wa kusimama katika kweli na haki, amani, upendo na kiasi."
Katika hitimisho la ujumbe wake, Dk Shoo amewashukuru waumini kwa upendo na ushirika wao katika kumtangaza Kristo na kuwatakia mwaka mpya wenye baraka.
Amesema anaamini 2026 utakuwa mwaka wa neema, mabadiliko chanya na mafanikio kwa Kanisa na Taifa la Tanzania kwa ujumla.
Wito wa Kiasi na Umoja
Mwinjilisti Lucy Kutema wa Usharika wa Moshi Pasua, amewahimiza waumini na Watanzania kutumia kwa kiasi katika sherehe na maisha ya kila siku, huku wakiwakumbuka na kuwasaidia watu wenye mahitaji.
Amesisitiza kuwa mwaka huu uwe wa kudumisha umoja, amani na mshikamano, ili kujenga jamii yenye mshikamano na heshima kwa wote.
"Mafanikio ya kufikia mwisho wa mwaka 2025 ni ushuhuda wa wazi kwamba ni mkono wa Mungu uliotubeba na kutulinda katika changamoto mbalimbali. Kwa msingi huo, ni vyema waumini kuishi maisha ya ibada, kumshukuru Mungu kila wakati na kutambua neema zake katika maisha yetu ya kila siku," amesema Mwinjilisti Lucy.
Aidha, Mwinjilisti Kutema amesisitiza umuhimu wa upendo ndani ya familia kama nguzo ya amani na ustawi wa familia, jamii na Taifa kwa ujumla. "Mungu ajalie mwaka 2026 uwe wa amani, furaha na mafanikio tele kwa kila mmoja," amesema.