Ajali ya Helikopta Katika Mlima Kilimanjaro Yaua Watu Watano
Moshi – Helikopta ya kampuni ya uokoaji ya KiliMediar Aviation imepata ajali maeneo ya kati ya Kibo na Barafu Camp katika Mlima Kilimanjaro na kusababisha vifo vya watu watano.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Kilimanjaro, Simon Maigwa, amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo leo Desemba 24, saa 11:30 wakati helikopta hiyo ilikuwa inatoka kuchukua wagonjwa wa kampuni ya utalii BobyCamping.
"Ni kweli kuna ajali ya helikopta ya kampuni ya uokoaji ya KiliMediar na waliofariki ni wageni wawili, muongoza watalii mmoja, rubani na daktari. Taarifa zaidi zitapatikana kesho asubuhi," amesema Kamanda Maigwa.
Taarifa kutoka eneo la tukio ambazo bado hazijathibitishwa zinaeleza kuwa baada ya helikopta hiyo kuanguka, ililipuka moto na kusambaratika huku jitihada za uokoaji zikifanyika.
Eneo la Kibo Hut na Barafu Camp liko kwenye urefu wa kati ya mita 4,670 na mita 4,700 kutoka usawa wa bahari.
Endelea kufuatilia TNC kwa taarifa zaidi…