CCM Yaanza Kufuatilia Ahadi za Viongozi, Waastaafu Waombwa Kustaafu kwa Heshima
Dodoma. Zikiwa zimekaribia kutimia siku 100 tangu Chama cha Mapinduzi (CCM) kichukue madaraka kwa awamu ya sita, uongozi wa chama hicho umetangaza kuanza rasmi kazi ya ufuatiliaji wa ahadi za viongozi wake ikiwemo alizozitoa Rais.
Mbali na hilo, chama hicho kikongwe barani Afrika kimewataka viongozi waliomaliza muda wao kustaafu kwa heshima ili waendelee kuwa msaada ndani ya CCM na Taifa.
Hayo yameelezwa na Katibu wa Itikadi, Mafunzo na Uenezi wa chama hicho, Kenani Kihongosi wakati akizungumza na waandishi wa habari Jijini Dodoma, Jumamosi, Januari 17, 2026.
Ufuatiliaji huo unakwenda kufanyika kupitia ziara za kiongozi huyo zilizopewa jina la Kliniki ya Kisiasa na zitaanza Januari 19 hadi 22, 2026 Mkoani Singida ambapo chama hicho kitakwenda kukutana na wananchi kwenye maeneo hayo ili kusikiliza kero na kuzitolea majibu.
Kihongosi amesema hatua hiyo inalenga kuhakikisha ahadi zilizotolewa wakati wa kampeni zinatafsiriwa kwa vitendo na kuwanufaisha wananchi katika sekta mbalimbali za maendeleo.
"Wajibu wetu ni kwenda kusikiliza umma unatuambia nini juu ya ahadi ambazo zimeanza kutekelezwa na zile ambazo bado, ila tuliahidi kuzitimiza ndani ya siku 100 hata kabla ya kutumia," amesema Kihongosi.
Kwa mujibu wa Kihongosi, CCM ina dhamira ya dhati ya kuwajibika kwa wananchi kwa kutekeleza kwa vitendo ilani yake, akisisitiza siku 100 za mwanzo ni kipimo muhimu cha mwelekeo wa Serikali mpya katika kutimiza matarajio ya wananchi.
Onyo kwa Viongozi Wastaafu
Kuhusu viongozi wastaafu, Kihongosi amewaonya baadhi kufuatia kauli wanazotoa ambazo zinaweza kuleta mgawanyiko ndani ya chama na Taifa kwa ujumla.
Kihongosi amesema viongozi wastaafu wanapaswa kutumika kama darasa la ushauri kwa viongozi wa sasa na si kulalamika au kukosoa uongozi wa sasa kwa namna isiyofaa.
"Kama chama tunaheshimu viongozi wetu wastaafu, tunawaambia wastaafu vizuri kama wastaafu wengine na waache ulalamishi na wasiwe na chuki kwa viongozi waliopo. Kama wanataka kutoa ushauri, utaratibu upo," amesema Kihongosi.
Ameongeza kwamba viongozi wastaafu wanapaswa kuendelea kuwa msaada na hazina ya busara kwa chama na Taifa badala ya kuwa chanzo cha migogoro na ugawanyiko.