Wananchi Waomba Serikali Kuharakisha Usajili wa Shule ya Sekondari Mondo Memusi Siha
Siha. Wananchi wa Kijiji cha Donyomurwak wilayani Siha, mkoani Kilimanjaro, wameitaka Serikali kuharakisha usajili wa Shule mpya ya Sekondari Mondo Memusi ili ianze kutoa huduma za elimu kikamilifu.
Ombi hilo limetolewa Januari 17, 2026, katika hafla ya ukabidhi rasmi wa shule hiyo kwa Serikali baada ya kukamilika kwa ujenzi wake katika Kijiji cha Oloiwang.
Wananchi wameeleza kuwa ujenzi wa shule hiyo umekuja kutatua changamoto kubwa iliyokuwa ikiwakabili wanafunzi waliolazimika kusafiri umbali wa kilometa 24 kila siku kwenda na kurudi kusoma katika Shule ya Sekondari Sekirari. Sasa ndoto ya watoto wao kupata elimu karibu na makazi yao imetimia.
Baada ya hafla ya makabidhiano, wananchi wameeleza kuwa kilichobaki ni Serikali kuharakisha usajili wa shule hiyo ili ianze kupokea wanafunzi haraka iwezekanavyo.
"Ombi letu kuu ni Serikali kusaidia kuharakisha usajili wa Shule ya Sekondari Mondo Memusi, ambayo inahudumia jamii ya wafugaji, ili ianze kufanya kazi kikamilifu kwa manufaa ya watoto wetu," mmoja wa wananchi amesema.
Mkazi wa eneo hilo, Paulina Israel, ameeleza kuwa hapo awali watoto walikuwa wakiamka saa kumi usiku kujiandaa kwenda shule kutokana na umbali mrefu. Hali hii ilisababisha uchovu, kuchelewa masomo na changamoto za kijamii, ikiwemo baadhi ya watoto wa kike kupata ujauzito wakiwa njiani au shuleni.
Kutokana na changamoto hizo, wananchi kwa kushirikiana na viongozi wao walianzisha ujenzi wa shule hiyo hadi hatua ya msingi, kabla ya kupata msaada wa kujenga vyumba vinne vya madarasa, ofisi mbili za walimu, matundu 12 ya vyoo kwa wanafunzi pamoja na meza na viti 100.
"Ujenzi umekamilika; kinachobaki ni usajili. Tunaomba Serikali ichukue hatua za haraka ili watoto waanze masomo," Paulina ameongeza.
Mkuu wa Wilaya ya Siha, Christopher Timbuka, amewahakikishia wananchi kuwa usajili wa shule hiyo utafanyika ndani ya mwezi wa Januari 2026, ili kuwezesha wanafunzi kuhamishwa kutoka Shule ya Sekondari Sekirari.
Mwenyekiti wa CCM wilayani Siha, Alfred Mosi, ameyapongeza mashirika yaliyoshiriki kwa kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuendeleza sekta ya elimu.
Mdau wa maendeleo wa wilaya hiyo, Mwalimu Meijo Laizer, ameeleza kuwa gharama ya jumla ya miradi ya elimu katika vijiji vya Donyomurwak na Oloiwang ni zaidi ya shilingi milioni 200, ikilenga kuboresha upatikanaji wa elimu na kuleta mabadiliko chanya kwa jamii.