Dar es Salaam. Watuhumiwa wawili wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Wilaya ya Temeke kwa tuhuma za kusafirisha dawa za kulevya aina ya Skanka zenye uzito wa kilo 20.
Watuhumiwa hao ni raia wa Msumbiji, Seleman Juma Ally (32) na Mtanzania, Amasha Iddi Mrisho (40), mkazi wa Buza, Dar es Salaam.
Washtakiwa walipandishwa kizimbani jana jioni, Alhamisi, Januari 22, 2026, na kusomewa mashtaka yao na Wakili wa Serikali Nicas Kihembe.
Kesi ya jinai namba 1535 ya mwaka 2026 imepangwa kusikilizwa na Hakimu Frank Lukosi katika hatua ya uchunguzi wa awali ili kukamilisha taratibu za msingi ukiwemo upelelezi kabla ya kuhamishiwa Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi ambayo ina mamlaka kisheria ya kusikiliza kesi kama hizi.
Kwa mujibu wa maelezo ya shtaka, watuhumiwa walikamatwa na maofisa wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) Desemba 8, 2025, katika mtaa wa Wailes, Temeke, Dar es Salaam.
Walikamatwa wakati maofisa wa DCEA wakifanya operesheni ambayo ilifanikisha kukamatwa pakiti 20 za dawa za kulevya aina ya skanka zenye uzito wa jumla wa kilogramu 20.03.
Dawa hizo zilikamatwa zimefichwa ndani ya balo la mitumba, ndani ya basi aina ya Scania la kampuni ya King Masai Tours, lenye namba za usajili wa Msumbiji AAM 297 CA.
Wakili Kihemba alieleza kuwa vitendo vya washtakiwa kukutwa wakisafirisha dawa hizo za kulevya ni kosa la jinai chini ya kifungu cha 16(I) cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya, inayokataza umiliki, usafirishaji na biashara ya dawa za kulevya nchini.
Wakili Kihemba aliiambia mahakama kuwa kulingana na uzito wa dawa waliokutwa nazo washtakiwa, shtaka hilo halina dhama.
Hata hivyo, wakili alieleza kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na akaiomba mahakama itoe ahirisho na kupanga tarehe nyingine ya kutajwa kama sheria inavyoelekeza.
Hakimu Lukosi aliahirisha kesi hiyo hadi Februari 5, 2026, itakapotajwa tena kwa ajili ya kuangalia mwenendo wa upelelezi na akaamuru washtakiwa wapelekwe mahabusu hadi tarehe hiyo.