Bei ya Bidhaa Yapanda Mbeya, Serikali Yaanzisha Uchunguzi
Mbeya – Kamati ya Ulinzi na Usalama Wilaya ya Mbeya, ikiongozwa na Mkuu wa Wilaya Solomon Itunda, imefanya ziara ya ghafla katika maduka na masoko ili kuchunguza ongezeko la bei za bidhaa zilizoshuhudiwa hivi karibuni.
Hatua hiyo imechukuliwa siku moja baada ya kuripotiwa kupanda kwa bei ya bidhaa mbalimbali jijini Mbeya, ikiwa ni sehemu ya jitihada za Serikali kudhibiti hali hiyo.
Kamati imeunda timu ya wataalamu 11 ambao wamekabidhiwa jukumu la kuchunguza chanzo cha kupanda kwa bei za bidhaa. Timu hiyo imepewa muda wa saa 72 kuwasilisha ripoti yao, ifikapo Jumatatu Januari 5, mwaka huu.
Ongezeko Kubwa la Bei Zasumbua Wananchi
Ripoti zinaonyesha kuwa bei ya mchele imepanda hadi Sh70,000 kwa kilo 20, sukari inauzwa Sh4,000 kwa kilo kutoka Sh3,000, na sabuni mche imefikia Sh4,200. Hali hii imezua malalamiko makali kutoka kwa wananchi wanaomtaka Serikali kuingilia kati haraka.
Leo Januari 2, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Solomon Itunda, akiambatana na viongozi mbalimbali, wataalamu na vyombo vya usalama, amefanya ziara katika baadhi ya maduka na kwa wafanyabiashara ili kujiridhisha na hali halisi ya masoko.
Serikali Yaonya Wafanyabiashara
Akizungumza wakati wa ziara katika soko la Mwanjelwa jijini Mbeya, Itunda amesema hatua hiyo imechukuliwa kufuatia malalamiko ya wananchi.
"Tumeunda timu ya watu 11 wakiwamo wajumbe kutoka vyombo vya usalama na wataalamu kutoka Halmashauri zetu za Mbeya Jiji na Mbeya DC. Tumewapa siku tatu ambapo Jumatatu wanapaswa kuwasilisha taarifa kwenye kamati ya usalama," amesema Itunda.
Ameongeza: "Baada ya ripoti hiyo itatusaidia kuwajua hao wafanyabiashara wasio waaminifu wanaamua kwa makusudi kuigombanisha Serikali na wananchi wake. Tutachukua hatua kwa watakaobainika kupandisha bei ya sukari na bidhaa nyingine."
Wafanyabiashara Waeleza Changamoto
Mfanyabiashara wa bidhaa za jumla na rejareja katika soko la Mwanjelwa, Andrea Mahenge, amesema kupanda kwa bei ya sukari hutokea kati ya miezi Machi hadi Juni kutokana na ukarabati wa viwanda.
"Hali hii hutokea mara chache sana na siyo kila siku. Asilimia kubwa huwa kati ya miezi fulani kuanzia Machi, Aprili, Mei na Juni kutokana na ukarabati wa viwanda," amesema Mahenge.
Muuza nyama, Nuhu Ambangile, amesema bei ya nyama imepanda hadi Sh11,000 kwa kilo kutokana na changamoto za malisho ya ng’ombe na gharama za usafirishaji.
"Mara kadhaa bei hupanda haswa kwa miezi hii kutokana na kukosekana kwa sehemu ya malisho. Wenye mifugo husafirisha vijijini na kufanya sisi wauza nyama kutumia gharama kubwa. Awali iliuzwa kilo moja Sh10,000," amesema Ambangile.
Muuza duka la rejareja, Triza Selestine, amesema bidhaa nyingi zimepanda ikiwamo unga wa ngano, akieleza kuwa suala la sukari limekuwa changamoto sana hadi kwenye maduka ya jumla.
"Kwa miezi miwili nyuma haikuwa bei sana. Ngano nayo imepanda kuanzia maduka ya jumla, hivyo hata mimi najikuta napata Sh1,000 katika mfuko," amesema Triza.
Mkuu wa Wilaya amewataka wananchi kuwa na uvumilivu kwa kipindi hiki kifupi ambapo baada ya ripoti na hatua zitakazochukuliwa, bei ya bidhaa zitarejea katika hali ya kawaida.