Waziri Mkuu Nchemba Atoa Wito wa Umoja na Amani kwa Watanzania
Dar es Salaam – Waziri Mkuu, Dk Mwigulu Nchemba ametoa wito kwa viongozi wa dini kuendelea kushirikiana na Serikali katika kutoa elimu ya umoja na amani, kupinga chuki, migawanyiko na vitendo vyovyote vinavyoweza kuvuruga mshikamano wa Taifa.
Amesema kuwa vita yoyote inayohusisha wenyewe kwa wenyewe huwa haina mshindi bali ina kupoteza wote na mgawanyiko ndani ya taifa hauna mshindi bali una matokeo ya kushindwa wote kama Taifa.
Dk Nchemba ametoa wito huo Ijumaa, Desemba 25, 2025 aliposhiriki ibada ya Sikukuu ya Krismasi iliyofanyika katika Kanisa Kuu la Kiinjili la Kilutheri la Azania Front jijini Dar es Salaam.
"Manufaa ya amani ni makubwa: huleta maendeleo ya kiuchumi, huimarisha ustawi wa jamii, na huwezesha kila Mtanzania kushiriki kikamilifu katika kujenga Taifa," amesema Waziri Mkuu.
Serikali Kuendelea Kulinda Amani na Usalama
Waziri Mkuu amesema kuwa Serikali inaendelea kutekeleza wajibu wake wa kulinda amani na usalama wa nchi pamoja na kuwajenga Watanzania na hususani vijana kuthamini dhana ya uzalendo kwa nchi yetu.
"Tanzania imeendelea kuwa kielelezo cha umoja, amani, mshikamano na utulivu katika ukanda wetu na barani Afrika. Amani hii imejengwa juu ya misingi imara ya maadili, haki, kuheshimiana, uvumilivu na uzalendo," amesema.
Pia, Dk Mwigulu ametoa wito kwa wazazi na walezi kuendelea kushirikiana kwa karibu na taasisi za elimu na dini katika kuimarisha malezi ya watoto na vijana kwa kuwajengea misingi imara ya maadili na kuwaongoza kutumia vyema fursa za elimu, teknolojia na utandawazi kwa maendeleo yao na Taifa kwa ujumla.
Ujumbe wa Krismasi
Katika ibada hiyo, Dk Mwigulu ameungana na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan kuwatakia Wakristo na Watanzania wote kwa ujumla, Heri ya Sikukuu ya Krismasi na kuwasishi kusherehekea kwa Amani, Upendo na Utulivu, kudumisha mshikamano wa Kitaifa kwa maslahi ya Taifa la Tanzania.
Mkuu wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT) na Mkuu wa Dayosisi ya Mashariki na Pwani, Askofu Dk Alex Malasusa amekemea tabia za baadhi ya watu za kuchafua taswira za watu wengine, pamoja na kuichonganisha jamii.
"Kuna watu wakiona jamii imekaa pamoja kwa amani wao inawakosesha raha," alisema Askofu Malasusa.