Mahakama Kuu Zanzibar Imachia Huru Mshtakiwa wa Mauaji
Arusha – Mahakama Kuu ya Zanzibar imemuachia huru Juma Suleiman Juma, aliyekuwa ameshtakiwa kwa kosa la mauaji ya Abdalla Haji Hamdu, baada ya Mahakama kujiridhisha kuwa hana kesi ya kujibu.
Mashtaka yalionyesha kuwa Septemba 30, 2024 katika eneo la Masingini, Mkoa wa Mjini Magharibi, Juma pamoja na watu wengine saba walimshambulia Abdalla kwa kumpiga kwa fimbo, kumvalisha tairi la gari, kummwagia petroli na kumchoma moto.
Abdalla alipelekwa Hospitali ya Mnazi Mmoja kwa matibabu ya dharura na baadaye kuhamishiwa Hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam. Kutokana na majeraha makubwa aliyopata, alifariki dunia Oktoba 5, 2024.
Hukumu ilitolewa Desemba 18, 2025 na Jaji Haji Suleiman Khamis aliyesikiliza kesi ya jinai namba 48/2024.
Uchunguzi wa mwili uliofanywa Oktoba 7, 2024 ulibaini kuwa marehemu alikuwa na majeraha makubwa ya moto yaliyofunika zaidi ya asilimia 80 ya mwili wake.
Upande wa Mashtaka Ulishindwa Kuthibitisha Kesi
Upande wa mashtaka ulitangaza kuwa ungekuwa na mashahidi 12 na vielelezo saba, lakini wakati wa usikilizaji uliita mashahidi wanne tu. Hao ni Haji Hamdu Ali (baba wa marehemu), Sada Abdulrahman Saleh (dada wa marehemu), Maryam Mussa Masoud (jirani wa marehemu) na Sajenti Hassan Kassim Mohamed, mpelelezi wa kesi.
Kumbukumbu za Mahakama zinaonyesha hakukuwa na vielelezo vilivyotolewa wakati wa kesi, ikiwa ni pamoja na ushahidi muhimu kama ripoti ya kifo, picha za eneo la tukio au ushahidi wowote wa kimatibabu.
Baada ya kusikiliza kesi ya upande wa mashtaka, Mahakama iliamua chini ya kifungu cha 263 (2) cha Sheria ya Mwenendo wa Jinai 2018 kuangalia kama ushahidi ulitosha kumfanya mshtakiwa awe na kesi ya kujibu.
Ukosefu wa Ushahidi Muhimu
"Baada ya kupitia ushahidi uliotolewa na mashahidi wa upande wa mashtaka, imebainika kuwa hakuna shahidi hata mmoja aliyemuona mshtakiwa akitenda kosa hilo au kushiriki shambulio dhidi ya marehemu," alisema Jaji.
"Zaidi ya hayo hakuna ushahidi wa kimatibabu uliowasilishwa mbele ya Mahakama, ripoti baada ya kifo ambayo ni msingi katika kuthibitisha ukweli wa chanzo cha kifo katika shtaka la mauaji, na zaidi hakuna kumbukumbu au vielelezo vilivyotolewa ikiwemo picha za eneo la tukio."
Jaji alisema kutokuwepo kwa ushahidi wa kimatibabu na wa kiuchunguzi hasa baada ya kifo ni hatari kwa kesi ya upande wa mashtaka.
"Mahakama hii inaona kwamba upande wa mashtaka umeshindwa kuanzisha kesi ya msingi dhidi ya mshtakiwa. Ushahidi uliotolewa hata kama utachukuliwa kwa kiwango cha juu zaidi haitoshi kumfanya mshtakiwa kujitetea."
Jaji aliamua: "Mshtakiwa anaonekana hana kesi ya kujibu, kwa hiyo ninaamuru aachiliwe huru isipokuwa kama ameshikiliwa kwa sababu nyingine."