Watafiti Watakabidhiwa Jukumu la Kukusanya Taarifa Sahihi za Haki za Binadamu Zanzibar
Unguja – Watafiti na wasaidizi wa kisheria wametakiwa kuhakikisha wanakusanya taarifa sahihi ili kupata matokeo halisi yatakayosaidia kuboresha utekelezaji wa haki za binadamu nchini.
Mkurugenzi Mtendaji wa Kituo cha Msaada wa Kisheria Zanzibar (ZLSC), Felista Mauya, amefungua rasmi mafunzo ya kuwajengea uwezo watafiti watakaoshiriki katika utafiti wa hali ya msaada wa kisheria na upatikanaji wa haki za binadamu visiwani Zanzibar, utakaofanyika mwezi huu.
Felista ameeleza kuwa lengo la utafiti huo ni kufanya tathmini na kupata taarifa za awali kuhusu viashiria vitakavyotumika kupima mafanikio ya utekelezaji wa haki za binadamu, hususan haki za kiraia na kisiasa, kiuchumi, kijamii na kiutamaduni.
Utafiti huo utaangalia namna haki hizo zinavyolindwa kisheria na vyombo mbalimbali visiwani Zanzibar, ili kubaini changamoto zilizopo na maeneo yanayohitaji kuimarishwa zaidi.
"Taarifa zitakazokusanywa zitaiwezesha ZLSC kupata uhalisia wa upatikanaji wa haki za binadamu na hivyo kuboresha mikakati ya utekelezaji kulingana na hali halisi katika kila wilaya za Zanzibar," amesema Mauya.
Hata hivyo, amewasisitiza watafiti hao kuzingatia ukweli na uadilifu wakati wa ukusanyaji wa taarifa hizo, ili kuepuka zile zinazopotosha umma na kuharibu taswira ya taasisi na nchi kwa ujumla.
Utafiti Utahusisha Watu 608
Castor Kalemera, mtafiti kiongozi wa haki za binadamu, amewaomba wananchi watakaofikiwa na utafiti huo kutoa taarifa za ukweli kwa masilahi ya jamii na taifa kwa ujumla.
Utafiti huo utahusisha watu 608 kutoka wilaya 11 za Zanzibar, wakiwemo wananchi wa makundi mbalimbali, watendaji wa Serikali, taasisi binafsi na asasi za kiraia.
Kalemera amesema utafiti huo utafanyika kwa kutumia mbinu mbalimbali ikiwamo ya mahojiano ya ana kwa ana na majadiliano ya vikundi, huku matumizi ya teknolojia yakizingatiwa kupata takwimu sahihi.
Matokeo ya Utafiti wa Awali
Akizungumzia utafiti wa awali uliofanywa na ZLSC mwaka 2024, Kalemera amesema uliwahusisha watu 300, matokeo yalionyesha kuwa asilimia 66 ya waliohojiwa waliripoti matukio ya ukiukwaji wa haki za binadamu kwa wakati katika mamlaka husika, asilimia 20 hawakuripoti na asilimia 14 hawakuwa na uhakika.
Asilimia 77 waliamini kuwa viongozi wao wanaheshimu na kulinda haki za binadamu, asilimia 14 walidai hawafanyi hivyo huku asilimia tisa wakisema hawakuwa na uhakika.
"Asilimia 72 walihisi wanafurahia uhuru wa kutoa maoni na kukusanyika, asilimia 25 hawakufurahia haki hiyo na asilimia nne hawakuwa na uhakika," amesema Kalemera.
Mshiriki wa mafunzo hayo, Halima AbdulKadir Mohamed, amesema katika utafiti uliopita walikumbana na changamoto ya ushiriki mdogo kutoka kwa baadhi ya wananchi.
Hivyo, amewaomba masheha kuwahamasisha wananchi ili kurahisisha upatikanaji wa taarifa sahihi kwa wakati.