Tanzania Inahakikisha Utalii na Amani Viko Imara Baada ya Machafuko ya Uchaguzi
Katibu Mkuu Wizara ya Maliasili na Utalii, Dk Hassan Abbas ameihakikishia dunia hali ya utalii na amani viko imara nchini Tanzania kufuatia maandamano yaliyozaa vurugu yaliyotokea wakati na baada ya uchaguzi mkuu Oktoba 29, 2025 katika baadhi ya maeneo.
Dk Abbas amesema hayo Novemba 9, 2025 alipoongoza ujumbe wa Tanzania katika Mkutano wa 26 wa Baraza Kuu la Shirika la Utalii Duniani (UN Tourism) jijini Riyadh, Saudi Arabia.
Amesema hayo wakati akichangia taarifa ya utekelezaji ya mwaka ya taasisi hiyo ambapo pia Tanzania ilinufaika na programu mbalimbali ikiwemo kuandaa Mkutano wa Dunia Kanda ya Afrika wa Utalii wa Vyakula uliofanyika Arusha Aprili 2025, na kufadhiliwa baadhi ya programu za utunzaji wa mazingira katika maeneo ya Safu za Milima ya Usambara.
"Mheshimiwa Mwenyekiti wa baraza hili baada ya kumpongeza Katibu Mkuu na sekretarieti ya UN Tourism kwa utekelezaji ambao Tanzania pia imenufaika, naomba kutumia fursa hii kutoa taarifa kuwa Tanzania ni salama baada ya kadhia iliyojitokeza wakati wa uchaguzi," amesema Dk Abbas.
"Serikali imefanya jitihada na kurejesha nchi yetu katika hali ya utulivu na hivyo kuendelea kuwa salama kwa watalii na vivutio vyetu vyote viko salama. Nawakaribisha wajumbe wa mkutano huu na wadau wengine wa utalii kuja na kuendelea kutembelea nchi hii ambayo ni kivutio bora Afrika kwa utalii wa safari," amesisitiza Dk Abbas.
Mkutano huo pamoja na mambo mengine utajadili kuhusu matumizi ya akili bandia katika kutangaza utalii na pia utachagua katibu mtendaji mpya.