Wizara ya Viwanda Yatangaza Mafanikio ya Siku 100 za Rais Samia
Dodoma – Wizara ya Viwanda na Biashara imetoa taarifa ya mafanikio ya siku 100 za Rais Samia Suluhu Hassan tangu kuapishwa kwa muhula wake wa pili, ikitaja mambo 12 ambayo yamepewa kipaumbele kikubwa hasa kwa kundi la vijana.
Katika utekelezaji wa mipango hiyo, mikopo 193 yenye thamani ya zaidi ya shilingi milioni 820 imetolewa na kusababisha uundaji wa ajira 546, ambazo nyingi zimewanufaisha vijana.
Waziri wa Viwanda na Biashara, Judith Kapinga alitoa takwimu hizo Jumamosi Januari 24, 2026 wakati wa mkutano na waandishi wa habari kuhusu mafanikio ya kipindi hicho.
Rais Samia Suluhu Hassan alitangazwa mshindi wa uchaguzi wa urais Novemba Mosi, 2025 na kuapishwa Novemba 3, 2025 katika viwanja vya Ikulu ya Chamwino, Dodoma.
Maeneo Makuu ya Mafanikio
Miongoni mwa mambo yaliyotajwa ni uwezeshaji wa wajasiriamali wadogo na wa kati, uendelezaji wa mitaa ya viwanda na programu maalumu za vijana.
Maeneo mengine ni pamoja na uongezaji wa thamani kupitia viwanda, uvutiaji wa uwekezaji wa viwanda na urasimishaji wa biashara na miliki ya ubunifu.
Kapinga alisema kuwa maeneo mengine yanajumuisha mafunzo na uatamizi wa biashara kwa vijana, ubora wa bidhaa kwa wajasiriamali, taarifa za masoko na biashara za kimataifa pamoja na uwezeshaji wa mauzo ya korosho.
Mikakati mingine inayotekelezwa ni muungano wa kampuni na ukuaji wa mitaji, utafiti wa madini adimu na ya kimkakati kupitia Tirdo, na uchumi wa kijani na nishati safi.
Uzalishaji wa Ajira
Waziri alieleza kuwa ndani ya siku hizo, mitaa ya viwanda na kongani zimezalisha maelfu ya ajira na kuandaa programu ya biashara 100,000 za vijana. Vijana 1,200 wamepata mafunzo ya ujasiriamali na kuingizwa kwenye programu za uatamizi wa biashara.
Miradi ya mpira Kalunga, mkaa mbadala na tafiti za madini adimu imeimarisha msingi wa uchumi wa kijani na uchumi wa kimkakati.
Udhibiti wa Biashara
Kuhusu maagizo ya Waziri Mkuu kuhusu biashara zinazoweza kuendeshwa na wazawa lakini zina wageni, Kapinga alisema wizara inaendelea kufanya ukaguzi wa mara kwa mara ikiwemo katika masoko makubwa ya Kariakoo.
"Brela wamepewa maelekezo wakati wa usajili wa biashara kuwa makini ili wasitoe usajili kwa wasiokuwa wazawa kwenye biashara ambazo zinaweza kumilikiwa na wazawa," alieleza Waziri.
Waziri ametaja sekta binafsi kuwa injini ya uzalishaji wa viwanda na kutoa ajira, na kusema Serikali inaendelea kutoa unafuu ili wakuze mitaji yao.