Mahakama Yahukumu Kifungo cha Miaka 28 kwa Kusafirisha Heroine
Dar es Salaam – Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi imemhukumu Isso Lupembe (55) kifungo cha miaka 28 gerezani baada ya kumtia hatiani kwa kosa la kusafirisha kilo 268.50 za dawa za kulevya aina ya Heroine.
Lupembe alikuwa anakabiliwa kesi ya uhujumu uchumi kwa shtaka moja la kusafirisha kilo 268.50 za dawa za kulevya aina ya Heroine, yeye na wenzake watatu, Allistair Mbele (43) mkazi wa Mbezi Kibanda cha Mkaa pamoja na raia wa Nigeria, David Chukwu (43).
Kwa mujibu wa hati ya mashtaka, walitenda kosa hilo Aprili 15, 2020 eneo la Mbezi Kibanda cha Mkaa.
Lupembe ametiwa hatiani baada ya kukiri shtaka hilo wakati wa usikilizwaji wa awali, ambapo Jamhuri iliwasomea hoja za awali kabla ya kesi hiyo kuanza usikilizwaji wa mashahidi wa upande wa mashtaka.
Hukumu Imetolewa na Jaji Otaru
Hukumu hiyo dhidi ya Lupembe imetolewa Januari 22, 2025 na Jaji Monica Otaru, baada ya Lupembe kukiri shtaka lake.
Wakati Lupembe akitiwa hatiani kwa kosa hilo kutokana na kukiri kwake, mshtakiwa mwingine Alistair Amon Mbele ameachiwa huru na Mahakama hiyo baada ya Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP) kumuondolea shtaka.
DPP ameieleza mahakama hiyo hana nia ya kuendelea na mashtaka dhidi ya mshtakiwa huyo kwa mamlaka aliyo nayo chini ya kifungu cha 92 (1) cha Sheria ya Mwenendo wa Mashauri ya Jinai (CPA), Marejeo ya mwaka 2023.
Hata hivyo, mshtakiwa wa kwanza katika kesi hiyo, David Chukwu (43) ambaye ni raia wa Nigeria hajakiri shtaka hilo, hivyo anaendelea na kesi hiyo.
Maelezo ya Mahakama
Mahakama imezingatia muda wa miaka mitano na miezi tisa ambao mshtakiwa amekaa rumande tangu alipokamatwa.
"Hivyo kutokana na hilo, mahakama imeelekeza kuwa atatumikia kifungo cha miaka 22 na miezi mitatu iliyobaki ili kukamilisha adhabu yake ya miaka 28," alisema Jaji Otaru.
Kuhusu mshtakiwa Mbele, Jaji Otaru alisema kuwa kwa kuwa DPP amewasilisha hati ya kutokuwa na nia ya kuendelea na mashtaka dhidi ya mshtakiwa huyo, mahakama hiyo inamuachia huru bila masharti.
Jaji Otaru alisema kuhusu mshtakiwa Chukwu ambaye hajakiri shtaka lake, kesi dhidi yake itaendelea Februari 23, 2025 kwa usikilizwaji, hivyo kwa kipindi hicho chote ataendelea kusalia rumande.
Maelezo ya Kesi
Katika kesi ya msingi, mshtakiwa aliyebakia anakabiliwa na kesi ya uhujumu uchumi namba 36 ya mwaka 2020.
Anadaiwa kutenda kosa hilo Aprili 15, 2020, eneo la Mbezi, Kibanda cha Mkaa.
Anadaiwa kuwa siku hiyo maofisa wa DCEA walimkamata yeye na wenzake wakisafirisha dawa za kulevya aina ya heroine zenye uzito wa kilo 268.50, kinyume cha sheria.
Kwa mara ya kwanza, washtakiwa hao walifikishwa katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Dar es Salaam, Kisutu Aprili 24, 2020 na kusomewa kesi ya uhujumu uchumi.
Kutokana na shtaka linalowakabili halina dhamana, washtakiwa hao walipelekwa mahabusu gerezani wakisubiri kesi yao kuamuliwa.