Wakurugenzi Waagizwa Kuwa Mfano wa Kupunguza Matumizi ya Plastiki
Dodoma – Wakurugenzi wa halmashauri nchini Tanzania wameagizwa kusimamia na kuwa mfano wa kupunguza matumizi ya plastiki katika ofisi zao ili kulinda mazingira.
Agizo hilo limetolewa Januari 17, 2026 na Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira, Profesa Peter Msofe wakati akizindua mradi wa urejeshaji wa mazingira na uoto wa asili.
Mradi huo wa miaka mitano unatekelezwa katika Wilaya za Mpwapwa na Chamwino (Dodoma) na Korogwe na Kilindi (Tanga).
Profesa Msofe amesema ni aibu wakurugenzi kuwa waangalizi kwenye uharibifu wa mazingira na hawatakiwi kuwa wapanga kazi badala yake wawe wasimamizi wa kazi hizo wakianzia wao kuonyesha mfano.
"Katika hili sitaki mkafanye, bali naagiza lazima litekelezwe tena iwe nchini nzima, na mshirikishe walio chini yenu na jamii inayowazunguka, lazima mtambue kwenye mazingira tuna hali mbaya na hivyo hatuwezi kucheka," amesema Profesa Msofe.
Kuhusu mradi huo amesema ni lazima uwe wa kiushindani katika mpango wa urejeshaji wa uoto wa asili ambapo Tanzania imejenga kufikia hekta milioni 5.2 wakati bara la Afrika ni hekta milioni 100 na kwa upande wa Dunia zinatakiwa kufikia hekta milioni 350 ifikapo 2050.
TNC imebaini kuwa lengo katika mradi huo ni kuboresha maisha ya wananchi na kulinda bayonuwai.
Mradi huo unagharimu Sh5.4 bilioni huku walengwa zaidi wakiwa watu wa vijijini katika wilaya zilizoonekana kuwa na uharibifu mkubwa wa mazingira.
Mradi uliopewa jina la IKI Forest Landscape unatekelezwa kwa nchi za Uganda, Madagasca, Brazil, Peru na Colombia.
Mkakati uliowekwa ni ufuatiliaji zaidi katika kila hatua ili kuhakikisha wanapata matokeo kama ilivyo.