Mbunge Patali Shida Azindua Juhudi za Kulinda Mazingira Mbeya
Mbeya – Mbunge wa Mbeya Vijijini, Patali Shida, ameahidi kuvalia njuga suala la utunzaji wa mazingira kwa kutoa elimu kuhusu athari za mabadiliko ya tabia nchi na kuhamasisha jamii kulinda vyanzo vya maji kwa maslahi ya vizazi vijavyo.
Hatua hiyo inalenga kutunza mazingira na kurejesha uoto wa miti ya asili iliyotoweka kutokana na shughuli za kibinadamu.
Mbunge huyo ametoa ahadi hiyo Januari 12, 2025, wakati akiwa mgeni rasmi kwenye zoezi la upandaji miti 1,000 kati ya 10,000, katika Kituo cha Afya cha Mamlaka ya Mji wa Mbalizi, Wilaya ya Mbeya.
"Kumekuwa na changamoto kubwa ya uharibifu wa mazingira hususani ukataji miti ovyo na uvamizi wa vyanzo vya maji. Katika hilo ninawataka wananchi kulinda rasilimali hizo kwa wivu mkubwa kwa maslahi ya vizazi vya sasa na baadaye," amesema.
Patali ameeleza kuwa ili nchi iwe salama katika masuala ya uchumi na mazingira, ni lazima kuelekeza nguvu katika upandaji wa miti na kupinga shughuli za ukataji wa miti kiholela hususani katika vyanzo vya maji.
"Jambo hili ninaendelea nalo katika maeneo mbalimbali kwenye ziara zangu. Najaribu kuwakumbusha wananchi kuishi katika misingi ya kutunza na kulinda mazingira ili kurejesha uoto wa miti ya asili," ameongeza.
Mbunge huyo ameomba vyombo vya habari kubeba ajenda hiyo na kutoa elimu kwa jamii kuhusu athari za kimazingira zitokanazao na uharibifu wa mazingira kwa kukata miti ovyo na kuvamia vyanzo vya maji kwa shughuli za kibinadamu.
Ofisa Maliasili na Utunzaji wa Mazingira Wilaya ya Mbeya, Gerald Shayo, amesema lengo la upandaji wa miti hiyo ni kurejesha uoto wa asili katika vyanzo vya maji na maeneo ya misitu yaliyoharibika, huku miti 10,000 ikipandwa maeneo mbalimbali.
"Lakini tunatoa tahadhari kwa wananchi kuachana na dhana ya kuchoma misitu kwa ajili ya kilimo kwani wanaangamiza miti mingi. Badala yake wailinde," amesema.
Shayo ameeleza kuwa asilimia kubwa ya misitu ya asili inachomwa hususani kwenye maeneo ya mipaka. Kutokana na hali hiyo, jamii inapaswa kubadilika kwa kuunga mkono jitihada za Serikali katika kuilinda kwa kugeukia kupanda miti ili kulinda vyanzo vya maji.
Mkazi wa Mamlaka ya Mji wa Mbalizi, Joyce Bakari, amesema ili kufikia malengo ya kutunza mazingira, umefika wakati wa elimu kutolewa na sheria kusimamiwa kikamilifu.
"Jamii bado haina uelewa juu ya utunzaji wa mazingira na uvamizi wa vyanzo vya maji kwa shughuli za kijamii hususani kilimo. Ni vizuri sasa watu wa mazingira kutoa elimu na kuvalia njuga sheria ili kukomesha," amesema.