Waziri Ridhiwani Kikwete Ataka Vijana Wawekeze Zaidi Kwenye Mfuko wa Faida
Dar es Salaam – Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejiment ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Ridhiwani Kikwete, ametoa wito kwa vijana kuwekeza zaidi katika mfuko wa faida ili kujiandalia mustakabali bora wa kifedha.
Mfuko huu ni mpango wa uwekezaji unaowapa Watanzania, hasa wenye kipato cha kati na chini, fursa ya kuwekeza katika vipande vya hisa na kupata mapato mazuri kupitia ukuaji wa mitaji. Lengo kuu ni kuendeleza utamaduni wa uwekezaji katika Masoko ya Fedha na Mitaji nchini.
Mpango huu unajumuisha wawekezaji wa kila aina, kuanzia wadogo kama vile madereva wa pikipiki, wanafunzi, wafanyakazi wa kawaida, wastaafu, wakulima, hadi wawekezaji wakubwa.
Akizungumza Jumamosi Januari 17, 2025, kwenye mkutano mkuu wa tatu wa mwaka wa uwekezaji wa FAIDA FUND ulioandaliwa na Watumishi Housing Investments (WHI), Waziri alisema kuwa uhamasishaji wa vijana ni jambo muhimu sana.
Vijana Wanahitaji Elimu ya Uwekezaji
Ridhiwani amesema kuna vijana wengi kutoka sekta mbalimbali ambao wamefanikiwa lakini wanahitaji mwongozo juu ya njia bora na salama za uwekezaji.
"Vijana hao pamoja na wafanyabiashara wakipata elimu sahihi ya uwekezaji, watawekeza zaidi kwenye mfuko huu ambao ni salama na wenye thamani," alisema.
Kulingana na taarifa ya usimamizi wa mfuko hadi Juni 2025, ukubwa wake umefikia shilingi bilioni 43.9 kutoka shilingi bilioni 25 mwaka uliopita, ikiwa ni ongezeko la shilingi bilioni 18.
Idadi ya Wawekezaji Inaongezeka
Ridhiwani alibainisha kuwa kwa sasa kampuni zaidi ya 200 zimewekeza kwenye mfuko huu huku idadi ya wawekezaji ikiongezeka kwa kasi. Aliitaka menejimenti kuendelea kukutana na taasisi mbalimbali ili Watanzania na kampuni nyingi zaidi ziwe sehemu ya wadau wakubwa wa mfuko huu.
"Kuna watumishi wa Serikali 1,200 wamewekeza. Idadi hii kwangu ni ndogo sana ukilinganisha na jumla ya watumishi wote wa umma. Nawahimiza kuchangamkia fursa hii ili kujiwekea akiba, uhuru wa kifedha na kujiandaa vizuri kustafu," alisema Waziri.
Aliitaka menejimenti ya mfuko huo kujitangaza zaidi na kutoa elimu kwa umma ili Watanzania wengi waweze kunufaika na fursa hii.
Mfuko Unazidi Kukua
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi wa WHI, Fortunatus Magambo, alisema mfuko huu unazidi kukua kwa kasi, jambo ambalo ni ishara ya maendeleo mazuri.
Alisema idadi ya wawekezaji imeongezeka kutoka 8,000 hadi 12,000, ikiwemo vijana wengi. Magambo alibainisha kuwa elimu ya uwekezaji inazidi kutolewa ili kuongeza uelewa na kuwavutia wawekezaji wengi zaidi kama alivyoshauri Waziri.
"Elimu ya kifedha inatolewa na itaendelea kutolewa hasa katika uwekezaji ili kupata wawekezaji wengi zaidi," alisema Magambo.