Chadema Yakabiliwa na Changamoto ya Ukosefu wa Wanawake Katika Nafasi za Uongozi
Dar es Salaam. Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) kikitimiza miaka 33 tangu kuanzishwa kwake, Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa chama hicho, Suzan Lyimo, ametoa taarifa kuhusu changamoto ya ukosefu wa wanawake katika nafasi za uongozi wa juu ndani ya chama.
Lyimo ameeleza kwamba nafasi muhimu za uteuzi ikiwemo Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu Tanzania Bara na Naibu Katibu Mkuu Zanzibar hazijawahi kushikwa na wanawake tangu chama kilipoanzishwa.
Akizungumza Januari 18, 2026, katika mjadala wa kidijitali kuhusu historia ya mabaraza ya Chadema, Lyimo alisema mjadala huo ni sehemu ya maadhimisho ya wiki ya kuanzishwa kwa chama ambacho kilele chake kinatarajiwa Januari 21, 2026.
Ameeleza kuwa hali hii inadhoofisha ushiriki wa wanawake katika uongozi wa juu, licha ya mchango mkubwa wanaoutoa katika kukijenga na kukiendesha chama.
"Tunaonekana kama wanawake wa ajabu, kwamba wanawake wa Chadema wana uwezo mkubwa lakini hawaonekani katika ngazi za juu za chama," amesema Lyimo.
Ameongeza kuwa ingawa katiba ya chama inaruhusu nafasi za kugombea, nafasi za uteuzi kama Katibu Mkuu na Manaibu Katibu Mkuu hazitolewi kwa wanawake.
Lyimo ameeleza jitihada zake za kuzungumza na viongozi wa chama ikiwemo Mwenyekiti Tundu Lissu na mwenyekiti wa zamani Freeman Mbowe, akitafuta suluhisho la changamoto hii wakati wa uchaguzi wa ndani uliofanyika Januari 21, 2025.
"Niliwaambia tumekuwa tukisemwa vibaya kwamba chama chetu kina mfumo dume. Niliwaomba yeyote atakayeshinda kwenye nafasi za uteuzi, angalau awepo mwanamke hata mmoja," ameeleza.
Hata hivyo, utekelezaji wa makubaliano hayo haukuwa kama ilivyotarajiwa. Lyimo amesema Lissu alieleza kuwa alikuwa tayari kuteua mwanamke, lakini mazingira yaliyokuwapo hayakumruhusu kutekeleza azma hiyo.
"Wanawake wa Chadema ni majasiri, wapewe fursa katika nafasi tano za juu. Kama tumekosa mwenyekiti au makamu mwenyekiti, basi hata katibu mkuu au naibu katibu mkuu bara au Zanzibar," amesisitiza.
Ameeleza kuwa nafasi hizo ni muhimu kwa wanawake kwa kuwa zinatoa mfano wa kuigwa, na kukosekana kwao katika uongozi wa juu kunawakatisha tamaa wanachama wengine.
Lyimo amewapongeza wanawake wa Chadema waliobaki imara ndani ya chama na kupitia changamoto mbalimbali.
Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa chama hicho, Sharifa Suleiman, amesema baraza lao linasimama imara katika kuongoza mapambano ya kupigania haki za msingi za Watanzania.