Simanjiro: Wanafunzi Waruhusiwe Kuanza Masomo Bila Sare za Shule
Simanjiro – Mkuu wa Wilaya ya Simanjiro (DC), mkoani Manyara, Fakii Lulandala amewaagiza walimu wakuu wa shule za msingi na sekondari kutowazuia wanafunzi kuanza masomo kwa sababu ya kukosa sare za shule.
Shule za msingi na sekondari nchini zimefunguka Januari 13, 2025, huku wanafunzi wapya wakianza masomo yao katika darasa la kwanza la shule za msingi na kidato cha kwanza kwa sekondari.
Lulandala, akizungumza Januari 16, 2025, amesema wanafunzi wanapaswa kupokelewe shuleni hata kama hawana sare, na hata wakijifunga mashuka ya asili (rubega).
Ameeleza kuwa suala la sare za shule litashughulikiwa baadaye, lakini kwa sasa jambo muhimu zaidi ni wanafunzi kuhudhuria masomo yao.
"Mwanafunzi asiye na sare asirudishwe kabisa, hata mmoja. Apokelewe endapo amevaa rubega pia ajiunge na shule. Wazazi na walezi watanunua nguo za shule baada ya watoto kuanza masomo," amesema.
DC Lulandala ameeleza kuwa lengo ni kuhakikisha asilimia 100 ya wanafunzi wote wanaopaswa kujiunga na elimu ya msingi na sekondari wanafika shuleni.
Hata hivyo, amewaagiza wazazi na walezi kutimiza wajibu wao na kutoipa mzigo serikali kwa kisingizio cha elimu bure.
"Suala la elimu bure halipo, ila kuna elimu bila malipo. Japokuwa majukumu ya serikali yapo yanafahamika na ya mzazi yanaeleweka," amesema.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halmashauri ya Wilaya ya Simanjiro, Gracian Makota ameahidi kusimamia utekelezaji wa agizo hilo la mkuu wa wilaya.
Makota ameeleza watahakikisha wanafuatilia wanafunzi wote wafike shule kwa asilimia 100 kama mwaka uliopita wa 2024.
Mkazi wa Kata ya Orkesumet, Esupaat Daniel amepongeza juhudi za mkuu wa wilaya katika kuhakikisha wanafunzi wanapata elimu.
Esupaat ameeleza kuwa mwaka jana wazazi na walezi walipeleka watoto wao shuleni wakihofia kuchukuliwa hatua kali na serikali.
Amesema hata wazazi na walezi waliokuwa na tabia ya kuozesha watoto wadogo kwa tamaa ya kupewa madume ya ng’ombe waliacha kwa kuhofia Serikali.