Unguja – Rais wa Zanzibar, Dk Hussein Ali Mwinyi, ametangaza uteuzi wa wakurugenzi watano kuwa wenyeviti wa bodi mbalimbali za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ikiwemo wastaafu wawili.
Taarifa rasmi iliyotolewa leo Jumatatu, Desemba 22, 2025 na Katibu Mkuu Kiongozi Zanzibar, Zena Ahmed Said, inaonyesha kuwa uteuzi huo unaanza rasmi leo.
Makame Hasnuu Makame, ambaye ni Mkurugenzi Mwendeshaji wa Shirika la Meli na Uwakala Zanzibar (Shipco), ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Usafiri Zanzibar (ZMA).
Sultan Said Suleiman, aliye Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Nyumba Zanzibar (ZHC), ameteuliwa kuongoza Bodi ya Wakurugenzi ya Shirika la Umeme la Zanzibar (Zeco).
Juma Burhani Mohamed, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Uwezeshaji Wananchi Kiuchumi Zanzibar (ZEEA), atakuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Zanzibar (ZAA).
Dk Maudline Cyrus Castico, Waziri Mstaafu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, ameteuliwa kuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Mamlaka ya Maji Zanzibar (Zawa).
Uteuzi huo pia unamshirikisha Dk Idrissa Muslim Hija, Katibu Mkuu Mstaafu wa SMZ, ambaye atakuwa Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya Wakala wa Karakana Zanzibar.