Serikali Yaahidi Alama ya Ubora kwa Wazalishaji wa Mwani Zanzibar
Unguja – Waziri wa Uchumi wa Buluu na Uvuvi Zanzibar, Masoud Ali Mohammed, ameahidi kuwapatia wazalishaji wa bidhaa za mwani alama ya ubora na uthibitisho, ili kuongeza thamani ya bidhaa hizo na kuimarisha uaminifu katika soko.
Waziri Masoud ametoa ahadi hiyo wakati wa ziara yake ya kukagua miradi ya uchumi wa buluu na uvuvi katika Mkoa wa Kusini Pemba Jumapili hii.
Hatua hiyo ni sehemu ya mkakati wa Serikali wa kuimarisha sekta ya mwani na kuwawezesha wazalishaji kuongeza thamani ya bidhaa zao.
"Serikali inatambua thamani ya zao hilo kwa wakulima ndio maana inafanya juhudi mbalimbali ili kuongeza tija kwao," amesema Masoud.
Waziri amesema Serikali itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali kuhakikisha wakulima wa mwani wananufaika zaidi kupitia utafiti, teknolojia na sera zinazowawezesha kuongeza kipato chao.
Ameeleza kuwa mafanikio ya sekta hiyo yanategemea nidhamu, ubunifu na mshikamano, huku akiwataka wanawake kujitokeza kwa wingi ili kunufaika na miradi hiyo na kujikomboa kiuchumi.
Sambamba na hilo, Waziri Masoud amesema Zanzibar inahitaji mageuzi makubwa ya kiuchumi kupitia sekta ya uchumi wa buluu na uvuvi, hatua itakayoimarisha uchumi na kuongeza ajira kwa wananchi.
Uimarishaji wa Miradi ya Uchumi wa Buluu
Naibu Waziri wa wizara hiyo, Mboja Ramadhan Mshenga, ameweka mkazo kuimarisha miradi na taasisi za uchumi wa buluu ili manufaa yake yawanufaishe wananchi wote.
Kwa upande wake, mkulima wa mwani, Ali Mbrouk Juma, amesema bidhaa zao zinakosa ubora kutokana na vifaa vinavyoharibika wanavyotumia.
Amesema Serikali ndio walezi kwa wakulima wote, hivyo ni wakati sahihi kujipanga vizuri katika kuwainua wakulima wa zao hilo.
Ziara ya Waziri Masoud ilijumuisha ukaguzi wa eneo linalotarajiwa kujengwa kiwanda cha kukata mwani na majongoo bahari Pemba, hatua inayotarajiwa kuongeza thamani ya mazao ya wakulima wa mwani nchini.