Kifo cha Mwanafunzi wa UDOM: Polisi Wachunguza Tukio la Kutumbukia Kisimani
Dodoma – Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wa kifo cha Said Kabuga, mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dodoma (UDOM), aliyefariki dunia kwa kutumbukia kisimani. Wanafunzi wenzake wameeleza kuwa kabla ya tukio hilo, alionekana mwenye mawazo akitaja fedha alizotumia kubeti.
Kabuga, ambaye alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa pili chuoni hapo, anatajwa kuwa ni mtu mpole na mkimya, ambaye hakupenda kujichanganya sana na wenzake, na hakuwa mhudhuriaji mzuri wa vipindi darasani.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Gallus Hyera, amesema taarifa za awali zinaonesha mwanafunzi huyo alijitupa kisimani kwa hiari yake.
Tukio hilo limetokea usiku wa kuamkia Jumatano, Novemba 26, 2025. Simu na vifaa vingine vimekutwa juu ya kisima hicho.
"Ni kweli taarifa hizo tunazo, lakini kinachoonesha ni kwamba alijitupa kisimani mwenyewe kwa kujiandaa, na bado kuna mambo tunayochunguza," amesema Kamanda Hyera.
Ushahidi wa Wanafunzi Wenzake
Ally Waziri, aliyekuwa karibu na Kabuga, ameeleza kuwa rafiki yake alikuwa mkimya na mwenye marafiki wachache, jambo ambalo huenda likawa sababu ya kutokufahamika kwa wanafunzi wengi.
"Ni rafiki yangu, nilifahamiana naye jeshini. Aliniambia ni mwenyeji wa Mkoa wa Tanga. Hakuwa na marafiki wengi kutokana na haiba ya upole aliyokuwanayo," amesema.
Waziri amesema tarehe 25 Novemba, Kabuga alionekana mchangamfu, lakini baadaye jioni alibadilika akawa mtu mwenye mawazo.
Mmoja wa wanafunzi ameeleza kuwa Kabuga alibeti fedha za ada, na baadaye alianza kulalamika kuwa itakuwaje kwa wazazi wake. "Hata chakula cha jioni hakula kutokana na hofu," amesema mwanafunzi huyo.
Jinsi Tukio Lilivyotokea
Wanafunzi wameeleza kuwa Kabuga alitoka usiku wakati wenzake walikuwa wamelala, akaenda eneo la kisima kilicho jirani, akaweka vifaa vyake na kujitumbukiza.
Ally Amani amesema alimuona Kabuga akielekea kisimani, huku akimulika kwa kutumia tochi ya simu akiwa na shati begani bila kifaa cha kubebea maji. Amesema kwa kawaida watu wanaokwenda kuchota maji kisimani hapo huwa na vyombo vya kuyabeba.
Muda mfupi baadaye, alisikia kelele, hivyo alishuka kutoka ghorofani na kuekekea kisimani, ambako alikuta simu na vifaa vya kusikilizia muziki vikiwa nje ya kisima hicho, huku mwanafunzi huyo akiwa ametumbukia ndani.
"Nilipofika pale, nilikuta simu, shati na vifaa vya kusikilizia muziki, ila yeye hakuwapo. Nikaenda kutoa taarifa kwa walinzi," amesema.
Baada ya walinzi kupata taarifa, walijaribu kumuokoa, lakini walishindwa kutokana na wingi wa maji kwenye kisima. Baada ya muda, askari walifika na kuopoa mwili wake.
Maoni ya Chuo Kikuu
Mkurugenzi wa Uhusiano UDOM, Rose Mdime, amesema kifo cha mwanafunzi huyo wamekipokea kwa mshtuko na simanzi.
Amesema chuo kimewaachia Jeshi la Polisi liendelee na uchunguzi.
"Tunatoa pole kwa familia, wazazi na wanafunzi wenzake kuhusu kifo hicho. Tunaomba wanafunzi wawe wapole na waliachia Jeshi la Polisi kufanya kazi yao," amesema.
Kabuga alikuwa mwanafunzi wa mwaka wa pili, akisoma Shahada ya Uandishi wa Habari na Uhusiano wa Umma.