Waziri Mkuu Mwigulu: Kampuni Changa Ndio Injini ya Kufikia Lengo la Uchumi wa Dola Trilioni Moja
Dar es Salaam – Waziri Mkuu Mwigulu Nchemba amesema Watanzania wanataka kuiona nchi yao ikifikisha lengo la uchumi wa kati wa Dola za Marekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050.
Dk Mwigulu amesema watakaofanikisha jambo hilo ni sekta binafsi ikiwemo wenye wabunifu kutoka kwenye kampuni changa.
Waziri Mkuu Mwigulu ametoa kauli hiyo leo Jumatano Desemba 3, 2025 wakati akifunga maadhimisho ya Wiki ya Kampuni Changa za Teknolojia kwenye ukumbi wa PSSSF, Makumbusho, jijini Dar es Salaam.
"Mtakumbuka kuwa Julai, mwaka huu Rais Samia Suluhu Hassan alizindua Dira 2050. Dira hii siyo ya Serikali peke yake bali ni kielelezo cha matarajio ya Watanzania ambao wanataka nchi yao ifikie uchumi wa kati wa dola za Marekani trilioni moja ifikapo mwaka 2050. Injini ya kuendesha nchi kuelekea maono haya ni sekta binafsi zikiwemo kampuni changa zinazoanzishwa," amesema.
Waziri Mkuu ambaye aliyekuwa akimwakilisha Rais Samia, amesema kazi ya kufikisha lengo siyo ndogo na inahitaji mabadiliko ya kiutendaji na kimtazamo. "Hatuwezi kufikia uchumi wa dola trilioni moja kwa kuendelea kuuza bidhaa ghafi au kufanya mabadiliko kidogo.
"Inatutaka tuwe na mbinu bunifu zenye tija: tuwe na njia mipya za kufanya mambo, tuanzishe makampuni mapya, tuwe na bidhaa mpya na teknolojia mpya zinazoweza kukua mara 10 badala ya asilimia 10," amesema.
"Inahitaji tuje na ubunifu wa Kitanzania utakaovutia mataifa na kuzalisha masoko ya nje. Inawezekana kabisa, twendeni tuunganishe nguvu," amesisitiza.
Amesema vijana waliochukua hatua ya kuanzisha kampuni changa wao ndiyo wenye hatima ya Tanzania na kwamba njia hiyo ndiyo sahihi ya kutenda kwa njia mbadala.
"Nchi nyingi za Afrika zinakabiliwa na changamoto ya vijana kutojiamini. Lakini wapo wengi ambao wametoa ajira kwa vijana wenzao. Na hii ndiyo njia sahihi ya kufanya mambo kwa njia mbadala kama ambavyo wenzeyu wamefanya," amesema.
Amewataka Watanzania waiheshimu sekta binafsi kama wanavyoiheshimu sekta ya umma kwa kuanza kubadilisha mtazamo wao ikiwemo nidhamu ya utendaji kazi.
"Kwa mazingira ya sasa, hakuna nchi imeweza kujenga uchumi mkubwa bila kuishirikisha sekta binafsi. Hiki mnachokifanya ndiyo injini ya kukuza uchumi," amesema.
Kampuni Changa Zaidi ya 1,000 Zimezalisha Ajira 140,000
Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Anjela Kairuki amesema Serikali imeendelea kuboresha mazingira ya kampuni changa ambapo hadi sasa kampuni changa za Kitanzania zinakadiriwa kufikia 1,041 na kuzalisha ajira zaidi ya 140,000.
Amesema hadi kufikia mwaka 2024, kampuni hizo zilikuwa zimeingiza mapato ya Dola za Marekani milioni 96.4 na kwamba hadi kufikia sasa zimekwishafikisha mapato ya dola za Marekani milioni 300.
Amesema kampuni nyingi zinazochipukia zimejielekeza kwenye matumizi ya teknolojia za huduma za kifedha, kilimo, afya, elimu na kwamba bado wanatarajia kuwa na bunifu nyingi za kidijitali.